BLOGGER TEMPLATES - TWITTER BACKGROUNDS »

Welcome - Karibu

Wedding Photography and Video

Friday 31 December 2010

Zanzibar For Democracy (U.K.)

Zanzibar For Democracy (U.K.) inachukua nafasi hii ili kuwapa pole na kuwafariji wanachama wa CUF na wananchi waliojeruhiwa na kukamatwa katika maandamano ya kuwasilisha rasimu ya katiba mpya; Wakati huo huo Jumuiya inawapongeza sana viongozi na wanachama wa CUF na wananchi waliojitolea kushiriki katika maandamano hayo na kufanikiwa kuiwasilisha rasimu hiyo.

Hatua hiyo waliyoichukua inathibitisha uelewa wao wa kiwango cha juu wa mapungufu yaliyomo katika Katiba iliyopo sasa ambayo haikidhi matakwa ya wananchi wengi wa Tanzania.
Tunaamini kuwa rasimu hiyo ni kielelezo halisi cha matakwa ya wananchi walio wengi na itakidhi kabisa hoja zote za kikatiba na kisheria ambazo kwa muda wote zimekuwa ni miongoni mwa matatizo ya msingi yanayoidhoofisha demokrasia nchini. Tunataraji kuwa hatua iliyochukuliwa na wananchi hao itakuwa ni changa moto muhimu sana kwa viongozi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika ngazi zote na kila mmoja wao ataikubali na kuitafsiri kuwa ni kichocheo cha kufungua kwa upana zaidi milango ya siasa za uwazi na kuwa ni dira kamili ya demokrasia iliyokamilika.

Tunaziomba taasisi zote za kiserikali na zile ambazo si za kiserikali kuunga mkono rasimu hiyo ili nchi yetu iweze kupata katiba mpya na tuachane na tabia ya kutia viraka kwani kufanya hivyo ni kuongeza matatizo badala ya kuyatatua. Aidha, tunawasifu sana wale wote walioiandika rasimu hiyo, kwani wao wameonyesha na kuthibitisha kwa vitendo namna wanavyoipenda na kuitakia mema nchi yetu. Tunawaomba wananchi wote waiunge mkono rasimu hiyo ili tuondokane na migogoro na mivutano inayokwamisha maendeleo.

Ahsante.

(Abdulla A. Abdulla), KATIBU, ZANZIBAR FOR DEMOCRACY(U.K.)


0 comments:

Search This Blog