BLOGGER TEMPLATES - TWITTER BACKGROUNDS »

Welcome - Karibu

Wedding Photography and Video

Monday 4 March 2013

TANESCO yakanusha kuwapo mgao wa umeme,yakusanya bilioni 2.3 kwa siku,yatumia bilioni 5.4

SHIRIKA la Ugavi wa Umeme Nchini (TANESCO) limekana kuwepo mgawo wa umeme kwa sasa huku likikiri kuwa hali ya upatikanaji wa nishati hiyo iko katika dharura na haijarejea katika hali ya kawaida kama inavyotakiwa.
Ufafanuzi huu unakuja baada ya gazeti hili kuripoti hali tete ya kifedha inayolikabili shirika hili na hivyo kutishia taifa kuingia gizani wakati wowote.
Hata hivyo TANESCO na serikali kupitia kwa Wizara ya Nishati na Madini wamekuwa kimya kwa muda pasipo kuzungumzia mgawo wa umeme ambao umekuwepo kwa wiki takriban mbili katika maeneo mengi nchini.
Akizungumza jana makao makuu ya shirika hilo Ubungo, jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Felchesmi Mramba, alisema kuwa hakuna mgawo wa umeme kwa sasa na kwamba ikitokea serikali ingetangaza.
Pamoja na kukanusha kuwepo kwa mgawo, Mramba alisema ukweli ni kwamba bado nchi iko katika hali ya dharura na hali ya umeme haijarejea katika hali yake ya kawaida kiasi cha kuondoka katika hali ya dharura.
“Ushahidi wa kwamba bado tuko katika hali ya dharura ni kwamba bado mitambo ya dharura tuliyokodi kupambana na hali ya umeme inaendelea kuhitajika lakini pia mabwawa hayana maji ya kutosha kukidhi mahitaji ya umeme bila kuhitaji mitambo ya matufa,” alisema.
Aliongeza kuwa vilevile miundombinu ya gesi haiwapi gesi ya kutosha kuwasha mitambo yote ya gesi ya megawati 501.
Mramba alibainisha kuwa tangu Julai mwaka 2012 hadi Februari 2013, serikali imetumia jumla ya sh bilioni 231.2 kama ruzuku kwa TANESCO kwa ajili ya kununua mafuta ya mitambo.
“TANESCO kutoka kwenye mapato yake imetumia jumla ya sh bilioni 423.3 katika kipindi hicho kununulia mafuta, hivyo fedha yote iliyotumika kununulia mafuta ndani ya kipindi hicho ni sh bilioni 654.5,” alisema.
Mramba aliongeza kuwa mitambo ya dharura inahitaji fedha nyingi kuiendesha kulinganisha na bei halisi ya kuuza umeme huo. Akitolea mfano alisema kuwa ili kuzalisha zinahitajika megawati 365 kwa mafuta (Dizeli-lita 1,368,00, HFO-LITA 500,000 na Jet A1-Lita 518,000 kwa siku.
Alisema kuwa jumla ya sh bilioni 5.4 zinahitajika kila siku au sawa na sh bilioni 162 kwa mwezi na kwamba mapato yanayotokana na kuuza asilimia 100 ya umeme wote unaozalishwa ni sh bilioni kwa siku sawa na takriban sh bilioni 70.2 kwa mwezi baada ya kuondoa kodi na tozo mbalimbali.
“Hata kama TANESCO ingeamua isilipe mishahara wala isifanye matengenezo ya mitambo, isinunue vifaa vya kuunganishia wateja, au isiingie gharama nyingine zozote, bado ingepata hasara ya karibu sh bilioni 90 kila mwezi,” alisema.
Mramba aliongeza kuwa kwa sababu kuna matumizi mengine muhimu ya kiuendeshaji, TANESCO inajikuta ikipata hasara kubwa zaidi kwa mwezi.
Kuhusu deni la Songas, mkurugenzi huyo alikiri kuwa ni kweli kampuni hiyo inaidai TANESCO na akasisitiza kuwa mkataba kati ya Songas na TANESCO unaruhusu hali hiyo.
Hata hivyo, kauli hiyo inatofautiana na kauli ya Naibu Waziri wa Nishari na Madini, George Simbachawene, aliyesema jana asubuhi kuwa wanaoshinikiza kuwa kuna deni kati ya Songas na TANESCO ni madalali tu.
Source:Tanzania Daima online

0 comments:

Search This Blog